ARUSHA-Bunge la Afrika Mashariki (EALA) Aprili 13, 2026 limefanya Mkutano Maalum katika makao makuu yake jijini Arusha, mkutano huo ulifanyika kwa njia ya mseto (ana kwa ana na kwa njia ya mtandao), ukiwaleta pamoja wabunge na wadau mbalimbali wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Moja ya matukio muhimu katika mkutano huo ni kuapishwa kwa Mheshimiwa Naibu Waziri wa wizara ya mambo ya nje na ushirikiano wa Afrika mashariki anayeshughulikia masuala ya Afrika Mashariki, James Kinyasi Millya, kuwa Mbunge wa Bunge la Afrika Mashariki (ex-officio).
Kwa mujibu wa Kanuni ya 5(4) ya Kanuni za Bunge la Afrika Mashariki, Mbunge haruhusiwi kushiriki katika shughuli za Bunge hilo bila kula kiapo cha utii kwa Mkataba wa Uanzishwaji wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Akizungumza mara baada ya kuapishwa, Mheshimiwa Millya amesema uteuzi na kuapishwa kwake ni ishara ya dhamira ya Serikali ya Tanzania kuendelea kushiriki kikamilifu katika kuimarisha ushirikiano wa kikanda.
“Naishukuru Serikali chini ya uongozi mahiri wa Mwanadiplomasia namba moja nchini, Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuniamini na nipo tayari kushirikiana na wabunge wenzangu kuhakikisha tunalinda na kuendeleza maslahi ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kwa manufaa ya wananchi wetu,” amesema Milya.
Aidha, ameongeza kuwa ataweka mkazo katika kuimarisha mtangamano wa Kikanda kupitia mshikamano miongoni mwa nchi wanachama, kukuza biashara ya kikanda pamoja na kusimamia utekelezaji wa sera na mikataba kwa ajili ya maendeleo ya Jumuiya yetu.Mkutano huo maalum pia ulijadili masuala mbalimbali ambayo yalilenga kuimarisha na kuboresha utekelezaji wa shughuli na programu ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.












