DAR-Mwenyekiti wa Tume ya Uchunguzi wa Matukio vurugu za Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 29, 2025, Jaji Othman Chande amekanusha uvumi wa kuwa Tume hiyo imeongezewa muda ili ripoti yao ichakachuliwe kwani tume hiyo haingiliwi na mtu yeyote yule, haina madalali.
Jaji Chande ametaja sababu za kuomba nyongeza ya muda wa siku 21 kuwa ni Ukubwa, Uzito, Kina cha kazi na ushahidi uliochelewa kuwafikia na ripoti hiyo kutakiwa kuandikwa kwa lugha mbili ya Kiswahili na Kingereza.
"Tume inajitegemea kwa kila kitu, tume yenyewe ndiyo Mhariri na yenyewe ndiyo msahihishaji. Mamlaka ambaye ametupa kazi tunaonana naye wakati tunatoa hadidu za rejea na wakati tunamkabidhi ripoti ya mwisho. Hatuna mtu yeyote katikati hapa, hatuna dalali."
Jaji Chande amesema, kwa sasa wanafanya kazi yao ya mwisho wakamilishe ripoti.Tume hiyo ilianza kutekeleza majukumu yake Novemba 20, 2025 na kutarajiwa kukamilisha kazi yake ndani ya kipindi cha siku 90.
Hata hivyo, kutokana na sababu mbalimbali, Tume iliongezewa muda wa kukamilisha kazi na kutakiwa kuwasilisha Ripoti kwa Rais kabla au ifikapo Aprili 3, 2026.
Hivyo, kufuatia nyongeza ya muda, wananchi waliendelea kujitokeza kwa wingi tofauti na matarajio ya Tume. Hivyo, Tume iliendelea kupokea ushahidi, taarifa na maoni zaidi.
Kwa sababu hiyo, Tume haikuweza kukamilisha kazi yake ndani ya muda wa nyongeza uliotolewa na hivyo kulazimika kuomba muda wa ziada ili kukamilisha kazi yake.
Aidha, tume imeendelea kuwashukuru wananchi na wadau wote waliotoa ushirikiano kwa Tume wakati wa kufanya uchunguzi, ikiwemo wale waliofika mbele ya Tume kutoa ushahidi, taarifa na maoni, waliopiga simu na kutuma ujumbe, waliotuma ushahidi, taarifa na maoni kwa maandishi na waliowasiliana na Tume kwa njia za mitandao ya kijamii.
