DODOMA-Viongozi mbalimbali akiwemo Naibu Waziri Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora Mhe. Regina Ndege, Katibu Mkuu Wizara ya Uchukuzi Prof. Godius Kahyarara, Mkurugenzi wa Taasisi ya Elimu ya Watu Wazima Prof. Philip L. Sanga na Mkurugenzi Mkuu Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA), CPA Dkt. Habibu Suluo pamoja na wananchi wametembelea banda la TRC katika maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yanayoendelea katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.
Katika maadhimisho hayo, TRC inaendelea kutoa elimu kwa wananchi kuhusu huduma za usafiri wa reli nchini, ikiwemo huduma za Treni ya Kisasa (SGR), huduma za usafirishaji wa mizigo na abiria, pamoja na fursa mbalimbali za uwekezaji na biashara zinazotokana na maendeleo ya sekta ya reli.
Aidha, wananchi wanapata nafasi ya kufahamu maboresho yaliyofanyika katika miundombinu ya reli, ratiba za safari, matumizi ya teknolojia za kisasa katika utoaji wa huduma, na mchango wa reli katika kuchochea ukuaji wa uchumi na maendeleo ya Taifa.
Maadhimisho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yamelenga kuwakumbusha watumishi uwajibikaji na kuchochea uwajibikaji jumuishi kwa huduma endelevu.




