GEITA-Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, SACP Safia Jongo, Julai 16, 2026, amefanya Baraza la Maafisa, Wakaguzi na Askari Polisi lililofanyika katika Ukumbi wa FFU Geita, ambapo amewapongeza askari kwa juhudi za kuendelea kulinda amani na kuimarisha ulinzi na usalama wa raia pamoja na mali zao katika Mkoa wa Geita.
Kamanda Jongo amesema kuwa hali ya usalama katika Mkoa wa Geita imeendelea kuwa shwari, huku akibainisha kuwa mafanikio hayo yanatokana na ushirikiano mzuri kati ya Jeshi la Polisi na wananchi. Amesema ushirikiano huo, pamoja na uwajibikaji, weledi na kujituma kwa askari katika kutekeleza majukumu yao kwa uzalendo, umeendelea kuimarisha ulinzi na usalama katika mkoa huo.
Kadhalika, amewataka Maafisa, Wakaguzi na Askari Polisi kuendelea kutekeleza majukumu yao kwa kuzingatia Kauli Mbiu ya Jeshi la Polisi inayosema, "Nidhamu, Haki, Weledi na Uadilifu," ili kuendelea kuimarisha utoaji wa huduma bora kwa wananchi, kuongeza imani ya wananchi kwa Jeshi la Polisi, pamoja na kudumisha amani, utulivu na usalama katika Mkoa wa Geita.









