NA GODFREY NNKO
BENKI Kuu ya Tanzania (BoT) imesema marekebisho ya Kanuni za Fedha za Kigeni za Mwaka 2026 yanawaruhusu wawekezaji wote wasio wakazi kuwekeza katika dhamana za Serikali za muda mfupi na muda mrefu zinazotolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Hayo ni kwa mujibu wa taarifa kwa umma iliyotolewa leo Agosti 6,2026 na Gavana wa Benki Kuu, Bw.Emmanuel M. Tutuba ambapo marekebisho hayo yamefanywa chini ya Sheria ya Fedha za Kigeni, Sura ya 271, kupitia Tangazo la Serikali Na. 206 la mwaka 2026 lililochapishwa katika Gazeti la Serikali la Julai 17, 2026.BoT imeeleza kuwa,kabla ya marekebisho hayo, ushiriki katika soko la dhamana za Serikali uliruhusiwa kwa wakazi wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) pamoja na Watanzania wanaoishi nje ya nchi pekee.
Kwa mujibu wa Benki Kuu, hatua hiyo inalenga kupanua wigo wa washiriki katika soko la dhamana za Serikali, kuongeza kina na ufanisi wa masoko ya fedha nchini, pamoja na kuimarisha nafasi ya Tanzania kama kitovu cha uwekezaji katika ukanda na kimataifa.
Aidha, Gavana Tutuba kupitia taarifa hiyo amefafanua kuwa,wawekezaji wasio wakazi sasa wataweza kuwekeza katika dhamana za Serikali kupitia mawakala wa uwekezaji waliothibitishwa, kwa kuzingatia masharti yaliyoainishwa katika Kanuni za Fedha za Kigeni (Marekebisho) za Mwaka 2026, pamoja na sheria nyingine husika na taratibu za kiutendaji zinazotolewa na Benki Kuu ya Tanzania.

