Cameroon yatwaa Ubingwa wa WAFCON kwa mara ya kwanza,yaichapa Malawi mabao 3-0

NA DIRAMAKINI

TIMU ya Taifa ya Wanawake ya Cameroon maarufu kama Indomitable Lionesses imeandika historia mpya baada ya kutwaa ubingwa wa Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) kwa mara ya kwanza, ikishinda Malawi kwa mabao 3-0 katika mchezo wa fainali uliochezwa Jumapili kwenye Uwanja wa Moulay El Hassan mjini Rabat.
Cameroon imeonesha kiwango bora katika mchezo huo na hatimaye kuvunja laana ya kupoteza fainali tatu zilizopita, baada ya mabao mawili ya Marie Ngah Manga na bao moja la Naomi Eto kuipa timu hiyo ushindi wa kishindo.

Mafanikio hayo yamekuja baada ya Cameroon kushindwa katika kila moja ya fainali zake tatu za awali za mashindano hayo, zote dhidi ya Nigeria ambayo ndiyo timu yenye mafanikio makubwa zaidi katika historia ya WAFCON ikiwa na mataji 10. Cameroon pia haikushiriki katika michuano iliyopita ya mashindano hayo.

Katika mtanange huo, Cameroon ilianza kuonesha makali yake dakika ya 21, wakati Ngah Manga alipofungua ukurasa wa mabao kwa kichwa baada ya kupokea nafasi ndani ya eneo la hatari.
Naomi Eto akaongeza presha kwa Malawi na kufunga bao la pili kupitia ustadi wa hali ya juu, akifanya mzunguko mzuri kabla ya kumalizia kwa ustadi na kuipa Cameroon uongozi wa mabao 2-0.

Aidha,Ngah Manga ambaye alikuwa katika kiwango bora alikamilisha ushindi wa Cameroon kwa bao lake la pili katika mchezo huo. Alifunga baada ya kuvunja safu ya ulinzi ya Malawi na kumalizia kwa kichwa kutokana na krosi ya Eto.

Bao hilo lilikuwa la tano kwa Ngah Manga katika mashindano hayo, likimfanya kuwa miongoni mwa wachezaji walioacha alama kubwa katika kampeni ya Cameroon kuelekea ubingwa.
Akizungumza baada ya ushindi huo, Ngah Manga amesema,mafanikio hayo yalikuwa kama ndoto kwao kutokana na muda mrefu ambao nchi yao ilikuwa ikisubiri mafanikio hayo.

“Nahisi kama ni ndoto kwa sababu Cameroon imekuwa ikifanya kazi kwa bidii ili kufikia wakati huu. Leo kuwa mabingwa wa Afrika ni jambo la ajabu sana kwetu,"amesema.

Licha ya kuanza kwa nguvu, Malawi ilishindwa kupata njia ya kupenya safu ya ulinzi ya Cameroon iliyocheza kwa nidhamu kubwa.
Malawi ambayo ilikuwa ikicheza fainali yake ya kwanza katika historia ya mashindano hayo, haikukata tamaa hadi dakika za mwisho. Hata hivyo, juhudi zake hazikuzaa matunda.

Viongozi wa FIFA na CAF washuhudia

Fainali hiyo imehudhuriwa na Rais wa Shirikisho la Kimataifa la Soka (FIFA), Gianni Infantino pamoja na Rais wa Shirikisho la Soka Afrika (CAF), Patrice Motsepe.
Viongozi hao wameshiriki katika hafla ya kukabidhi medali baada ya mchezo huku wakipiga picha pamoja na Rais wa Shirikisho la Soka la Cameroon, Samuel Eto’o na mchezaji bora wa mashindano hayo,Monique Ngock.

Katika mchezo wa kuwania nafasi ya tatu uliochezwa Jumamosi, Algeria iliifunga wenyeji Morocco na kumaliza mashindano hayo katika nafasi ya tatu.
Aidha,kwa Cameroon, ushindi huo umefungua ukurasa mpya katika historia yake ya soka la wanawake, baada ya miaka ya kusubiri na maumivu ya kupoteza fainali, ambapo Indomitable Lionesses sasa wanaondoka Rabat wakiwa mabingwa wa Afrika kwa mara ya kwanza.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Know matter how large or small your business is, advertising here