Nigeria na Ghana waikataa Afrika Kusini

NA DIRAMAKINI

SERIKALI ya Afrika Kusini imeingia katika mvutano wa kidiplomasia na baadhi ya nchi za Afrika baada ya kutaka kurejeshewa takribani dola milioni 18.5 (rand milioni 292.77) ilizotumia katika shughuli za kuwarejesha nchini kwao raia wa kigeni waliokuwa nchini humo.
Picha na Al Jazeera.

Idara ya Mambo ya Ndani ya Afrika Kusini imesema,gharama hizo zimezidi kwa kiasi kikubwa bajeti yake ya rand milioni 60 iliyotengwa kwa ajili ya kuwafukuza na kuwarejesha wahamiaji wasio na hadhi halali nchini humo.

Kwa mujibu wa serikali ya Pretoria, ongezeko kubwa la shughuli za utekelezaji wa sheria za uhamiaji limesababisha gharama za usafirishaji,malazi,watumishi na shughuli nyingine za uendeshaji kupanda zaidi ya makadirio ya awali.

Serikali hiyo imesema inataka kurejeshewa fedha hizo na baadhi ya nchi za Afrika ambazo raia wake walirejeshwa kutoka Afrika Kusini.

Nchi zilizotajwa wazi na Pretoria ni Nigeria, Malawi na Ethiopia. Idara ya Mambo ya Ndani imesema,iliwasiliana na Serikali ya Malawi pamoja na balozi za Nigeria na Ethiopia kupitia Idara ya Uhusiano na Ushirikiano wa Kimataifa (DIRCO) ikiomba kurejeshewa gharama hizo.

Hata hivyo, Nigeria imekanusha kupokea ombi rasmi la malipo kutoka Afrika Kusini. Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Nigeria, Kimiebi Imomotimi Ebienfa, alinukuliwa na BBC akisema Abuja haijawahi kupokea ombi hilo.

“Hatujawahi kupokea ombi lolote,” alisema Ebienfa. Kauli hiyo imeibua tofauti kati ya maelezo ya Pretoria, inayodai kuwa mawasiliano ya kudai marejesho ya fedha yamewasilishwa kupitia njia za kidiplomasia, na msimamo wa Abuja unaosema hakuna ombi kama hilo lililofikishwa katika wizara yake ya mambo ya nje au katika ubalozi wake.

Wakati huo huo, Ghana imejitenga na madai hayo, ikisema haipaswi kulipa Afrika Kusini gharama zozote zinazohusiana na kurejeshwa kwa raia wake.

Katika taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje ya Ghana, Accra ilisema imefahamu madai ya Afrika Kusini ya kutaka takribani dola milioni 18 kutoka kwa nchi kadhaa za Afrika kwa gharama za msaada na uratibu uliotolewa wakati wa kuwaondoa raia wa kigeni.

Hata hivyo, Ghana ilikataa vikali wazo kwamba Afrika Kusini inapaswa kurejeshewa fedha kwa ajili ya kuwaondoa raia wa Ghana.

Kwa mujibu wa wizara hiyo, gharama zote za kuwaondoa raia wa Ghana zililipwa na Serikali ya Ghana pamoja na washirika wake wa Ghana.

“Ghana haikuomba msaada wa kifedha wala wa vifaa kutoka Serikali ya Afrika Kusini ili kuwarejesha raia wetu nchini,”ilieleza taarifa hiyo.

Serikali ya Ghana pia imewahakikishia raia wake kwamba haitahusishwa na orodha ya nchi ambazo Afrika Kusini inataka zirejeshe gharama za kuwarejesha raia wake.

Kauli za Ghana na Nigeria zinaongeza shinikizo kwa Pretoria wakati Serikali ya Afrika Kusini ikikabiliwa na mzigo mkubwa wa kifedha unaotokana na kuongezeka kwa operesheni za kudhibiti uhamiaji na kuwarejesha wahamiaji nchini mwao.

Afrika Kusini imeeleza kuwa,matumizi ya rand milioni 292.77 ni takribani mara tano ya bajeti yake ya awali ya rand milioni 60 kwa shughuli za kuwafukuza na kuwarejesha wahamiaji.

Ongezeko hilo linaakisi changamoto inayokabili mamlaka za Afrika Kusini katika kudhibiti uhamiaji haramu huku idadi ya operesheni za ukamataji na urejeshaji wa raia wa kigeni ikiongezeka.

Aidha,gharama hizo zinahusisha usafiri wa kuwapeleka wahusika katika nchi zao, malazi, ulinzi na watumishi pamoja na mahitaji mengine ya kiutendaji yanayohusiana na mchakato wa repatriation.

Hata hivyo, msimamo wa Ghana na Nigeria unaonesha kuwa suala la nani anayepaswa kubeba gharama hizo linaweza kuendelea kuwa changamoto ya kidiplomasia kati ya Pretoria na mataifa mengine ya Afrika.

Kwa sasa, tofauti kubwa iko katika tafsiri ya wajibu wa kifedha, kwani Afrika Kusini inataka nchi za asili za baadhi ya raia waliorejeshwa zichangie gharama, huku Nigeria ikisema haijapokea madai rasmi na Ghana ikisisitiza kuwa iligharamia yenyewe zoezi la kuwaondoa raia wake.

Mvutano huo unatarajiwa kuongeza mjadala mpana kuhusu namna nchi za Afrika zinavyopaswa kushirikiana katika kushughulikia uhamiaji, utekelezaji wa sheria za mipakani na gharama za kuwarejesha wahamiaji katika nchi zao.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Know matter how large or small your business is, advertising here