DAR-Mtengeneza maudhui anayefahamika kwa jina la Somadian Nunez amemuomba msamaha Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wanawake na Makundi Maalum, Mhe. Dkt. Dorothy Gwajima pamoja na Watanzania kwa ujumla, kufuatia maudhui aliyokuwa akiyasambaza mitandaoni ambayo yalikosolewa kwa kukiuka maadili ya jamii.
Hatua hiyo imekuja baada ya Dkt. Gwajima kumuonya kijana huyo kuacha kutumia lugha ya matusi na kuwahusisha watoto katika maudhui yasiyofaa, huku akimtaka kuyaondoa maudhui hayo na kubadilisha mwenendo wake kabla sheria haijachukua mkondo wake.
Akizungumza kuhusu hatua hiyo,Somadian amesema amepokea wito wa Waziri na tayari ameondoa maudhui hayo kwenye akaunti yake ya TikTok. Pia amewaomba msamaha wote ambao huenda waliwahi kukwazwa na maudhui yake, huku akiahidi kubadilika na kuzingatia maadili katika matumizi yake ya mitandao ya kijamii.
“Mama yangu Waziri Gwajima na Watanzania kwa ujumla, naomba mnisamehe kijana wenu. Nimebadilika,”amesema Somadian.
Aidha, amewataka watu wanaotumia jina lake au kusambaza video zake kwenye TikTok kuondoa maudhui yasiyofaa, akisisitiza dhamira yake ya kubadilika na kuwa mfano bora kwa jamii.
Kwa upande wake,Waziri Gwajima amesema, amemsamehe kijana huyo na kumtaka kutumia uwezo wake wa kutengeneza maudhui yenye tija kwa jamii na yatakayomsaidia kujenga maisha na mustakabali wake.
