Tanzania na Marekani zaahidi kuendeleza ushirikiano katika nishati,afya na uwekezaji

DAR-Tanzania na Marekani zimeendelea kusisitiza umuhimu wa kuimarisha ushirikiano wa kimkakati katika sekta mbalimbali zikiwemo madini adimu, nishati, afya, uwekezaji na maendeleo ya kiuchumi, pamoja na dhamira ya kuendeleza mazungumzo na ushirikiano wa kitaalamu kwa manufaa ya nchi hizo mbili.
Hayo yameafikiwa na Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) na Kaimu Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Mhe. Andrew Lentz, walipokutana na kufanya mazungumzo ya katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha, jijini Dar es Salaam, ambapo pia walieleza umuhimu wa kuendelea kutumia majadiliano ya kitaalamu na ushirikiano wa Serikali kwa Serikali katika kushughulikia maeneo yenye umuhimu wa kimkakati, ikiwemo maendeleo ya sekta ya Nishati ya Gesi Asilia (Liquefied Natural Gas (LNG).

Kaimu Balozi wa Marekani nchini Tanzania, Mhe. Andrew Lentz, alisisitiza kuwa mawasiliano ya karibu na ushirikiano kati ya wataalamu wa pande zote ni muhimu katika kuwezesha utekelezaji wa miradi mikubwa ya kimkakati.

Aidha, walijadili fursa za kuendelea kuimarisha mazingira ya uwekezaji nchini, ikiwemo miradi mikubwa ya madini na kuongeza thamani ya rasilimali nchini, ambapo walikubaliana kuhusu umuhimu wa kuwa na uratibu mzuri wa Serikali na wawekezaji ili kuhakikisha miradi ya kimkakati inatekelezwa kwa ufanisi na kutoa manufaa kwa uchumi na wananchi.
Kwa upande wa afya, alisema kuwa hivi karibuni, Marekani na Tanzaniaa zimesaini makubaliano ya kuendeleza sekta ya afya yatakayogharimu dola za Marekani bilioni 3.1 katika kipindi cha miaka mitano ijayo kwa ajili ya kuimarisha mifumo ya afya, kukabiliana na magonjwa mbalimbali na kujenga uwezo wa ndani, kuelekea kwenye mifumo endelevu ya afya inayoongeza uwezo wa Tanzania kugharamia na kusimamia huduma za afya kwa muda mrefu, sambamba na kuimarisha uwezo wa kitaifa katika kinga, ufuatiliaji na udhibiti wa magonjwa.
“Tunatambua umuhimu wa uwekezaji katika miundombinu ya afya, uzalishaji wa bidhaa za afya nchini na kuimarisha taasisi zinazohusika na afya ya umma na Ushirikiano huu unalenga kuongeza uwezo wa Tanzania kukabiliana na changamoto za kiafya na kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora na endelevu,”alisema Mhe. Balozi Lentz.

Kwa upande wake Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), alisema kuwa kuna nafasi kubwa ya kubadilishana uzoefu kuhusu namna Serikali hizo zinavyoweza kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi, kifedha na kitaalamu, na Serikali inatambua juhudi zinazoendelea za wataalamu wa pande zote mbili katika kuimarisha mifumo ya kifedha, ikiwemo maendeleo ya soko la dhamana za Serikali, ambazo zinatajwa kama mfano wa ushirikiano wa kitaalamu unaoweza kutoa manufaa ya muda mrefu kwa uchumi wa Tanzania.
“Kwa ujumla, mkutano huu umeonesha dhamira ya Tanzania na Marekani ya kuendeleza ushirikiano wa karibu katika maeneo ya kimkakati, na msisitizo mkubwa ukiwa katika kuimarisha uwekezaji, kujenga uwezo wa ndani, kuongeza thamani ya rasilimali na kuhakikisha ushirikiano huo unaleta matokeo chanya na endelevu kwa wananchi,”alisema Mhe. Balozi Omar.

Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Kamishna wa Idara ya Usimamizi wa Deni la Serikali, Wizara ya Fedha, Bw. Japhet Justine, Mkurugenzi Msaidizi wa Huduma za Sheria Wizara ya Fedha, Bi. Mwantumu Sultan, Mshauri wa Siasa na Uchumi Ubalozi wa Marekani Nchini, Bi. Rebecca Hunter, na wataalamu wengine wa Wizara ya Fedha na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Know matter how large or small your business is, advertising here