NA DIRAMAKINI
JESHI la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam linamshikilia Conrad Agonza Kayoza mkazi wa Lugalo na Mloganzila jijini Dar es Salaam kwa kumshambulia kwa ngumi na mateke Askari wa Kikosi cha Usalama Barabarani.
Hayo ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo Septemba 8,2026 na Kamanda Kanda Maalum ya Polisi Dar es Salaam,Muliro Jumanne Muliro
Kamanda Muliro amesema, leo Septemba 8,2026 majira ya saa 1:30 asubuhi huko eneo la Lugalo Kinondoni jijini Dar es Salaam katika barabara ya Bagamoyo, Askari Polisi namba F. 8886 SGT Andrew wa Kikosi cha Usalama Barabarani Kinondoni wakati anatekeleza majukumu yake alishambuliwa kwa ngumi na mateke na mtu huyo.
"Askari huyo alikuwa kazini na aliyazuia kisheria magari yaliyokuwa yakipita pembezoni mwa barabara "Service Road" nje ya utaratibu likiwemo gari la mtuhumiwa lenye namba T 455 EER aina ya Toyota Runx ndipo mtuhumiwa alishuka kwenye gari na kuanza kumshambulia askari kabla na yeye mtuhumiwa kushambuliwa na wananchi waliochukizwa na kitendo hicho.
"Mtuhumiwa Conrad Agonza Kayoza amepelekwa hospitali kwa matibabu na akipata nafuu atahojwa kwa kina ili hatua za kisheria zichukuliwe na mamlaka zingine za kisheria."
Vilevile,Polisi Dar es Salaam wametoa tahadhari na onyo kali kuwa halitavumilia wala kusita kuchukua hatua kali za kisheria na za haraka kwa mtu yeyote au kundi litakalo shambulia Polisi wakati wakiwa wanatekeleza majukumu yao ya kisheria.

