NA DIRAMAKINI
WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais,Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete amepongeza maandalizi ya Mkutano Mkuu wa Chama Cha Watunza Kumbukumbu na Nyaraka (TRAMPA), akisema mkutano huo unatarajiwa kuwa chachu ya kuimarisha chama hicho pamoja na tasnia ya utunzaji wa kumbukumbu na nyaraka nchini.
Ameyasema hayo leo baada ya kupokea taarifa ya maandalizi ya Mkutano Mkuu wa TRAMPA kutoka kwa Mwenyekiti wa chama hicho,Bi. Devotha Mrope aliyefika ofisini kwake Mtumba, Dodoma, akiwa pamoja na Kamati Tendaji ya chama.Mheshimiwa Ridhiwani Kikwete amesema, amefurahishwa na hatua zilizofikiwa katika maandalizi ya mkutano huo, huku akiwapongeza viongozi wa TRAMPA kwa kazi nzuri waliyoifanya hadi sasa.
“Nimepokea taarifa ya maandalizi ya Mkutano Mkuu wa Chama Cha Watunza Kumbukumbu na Nyaraka (TRAMPA) ofisini kwangu Mtumba, Dodoma, kutoka kwa Mwenyekiti wa Chama hicho, Bi. Devotha Mrope, alipofika kuniona pamoja na Kamati Tendaji yao,” amesema Waziri Kikwete.
“Nikizungumza baada ya kupokea taarifa hiyo, nimewapongeza kwa kazi nzuri ya maandalizi na tunatarajia mkutano mzuri unaolenga kuimarisha chama chao na tasnia yao.”
Mkutano huo unatarajiwa kujadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo na uimarishaji wa TRAMPA pamoja na tasnia ya utunzaji wa kumbukumbu na nyaraka.
TRAMPA ni chama kinachowakutanisha na kuwaunganisha wataalamu na watunza kumbukumbu,nyaraka na masijala kutoka sekta ya umma na binafsi nchini.
