Waziri Mkenda, Kundo wampa kongole Mathias Canal kwa kuanzisha WazoHuru Media Group Limited,yazinduliwa

NA INNOCENT NATAI

WAZIRI wa Elimu Sayansi na Teknolojia,Mhe. Prof. Adolf Mkenda (Mb) amewataka vijana wa kitanzania kujenga utamaduni wa kujiajiri na kuwa wabunifu ili kuisaidia Serikali kupunguza kundi la wasio na ajira.
Ametoa rai hiyo Novemba 4, 2022 wakati akizungumza kwenye uzinduzi wa Kampuni ya WazoHuru Media Group Limited inayomilikiwa na Mathias Canal, uliofanyika mtaa wa Swaswa, Kata ya Ipagara jijini Dodoma.

Waziri Mkenda amesema kuwa, mpaka sasa Serikali imepiga hatua kubwa katika kuwajengea vijana uwezo wa kujiajiri ambapo uzinduzi wa kampuni hiyo inayojihusisha na masuala ya habari, kijana Mtanzania amewekeza hivyo ameongeza chachu kwa vijana wengine kuona ni namna gani wanaweza kuajiriwa huku wamejiajiri na kuajiri vijana wengine.
“Sisi watanzania tuongeze bidii ya kufurahia mafanikio ya wenzetu, tukiona mwenzetu mwenye ndoto anafanikiwa tunamuunga mkono kwa kumuombea na kumtakia kila la heri na tumekuja hapa na wabunge kuunga mkono jitihada hizi,”amesema Prof.Mkenda.

Awali akimkaribisha mgeni rasmi Naibu Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe Mhandisi Mathew Kundo amempongeza Mtendaji Mkuu wa WazoHuru Media Group Limited, Mathias Canal kwa kuhakikisha anafuata sheria na kanuni za uanzishwaji wa Kampuni na Kituo cha Habari kama yalivyo matakwa ya kisheria.
Baada ya mapinduzi ya teknolojia badala ya kusubiri taarifa kwenye televisheni ya nyumbani sasa tunaruhusu watu kuwa na televisheni ya mtandaoni na mwananchi anaweza kupata habari kupitia simu yake ya mkononi. "Na hapa leo tumezindua televisheni ya Mtandaoni ni jambo kubwa kama wizara tunaahidi kuwapa ushirikiano wa kutosha,"amesema

Pia ameongeza kuwa, amefurahishwa na kuona kijana wa kitanzania anajiajiri na kuweza kuajiri vijana wengine ili kuhakikisha wanajipatia kipato na kuwezesha upatikanaji wa habari na elimu kwa jamii kwa urahisi.
Akitoa taarifa ya kampuni mbele ya mgeni rasmi, Afisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya WAZOHURU MEDIA GROUP LIMITED,Mathias Canal ameiomba serikali kuona namna ya kuwawekea mazingira mazuri vijana waliosomea masuala ya Habari na mawasiliano ya kujiajiri kwa kumiliki vyombo vya habari ambavyo vitarahisisha upatikanaji wa taarifa za kitaalamu na ujuzi kwa jamii.

Ameongeza kuwa, mpango wa kampuni hiyo iliyojipambanua katika masuala ya Habari na mawasiliano ilianza kupitia kundi la WhatsApp Mkoani Iringa mwaka 2014 na baadae kuanzisha televisheni ya Mtandaoni (Youtube Tv) pamoja na Blog.

Canal amesema kuwa, malengo ya kampuni hiyo ni pamoja na kuanzisha gazeti litakalofahamika kama WazoHuru, kuanzisha kituo cha redio itakayofahamika kama WazoHuru Fm na Televisheni itakayofahamika kama WTV.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news