Ujenzi Mji wa Serikali waneemesha wengi kiuchumi

DODOMA-Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu anayeshughulika na (Sera, Bunge na Uratibu),Mhe.Jenista Mhagama amesema, mradi wa ujenzi wa Mji wa Serikali Mtumba pamoja na miradi mingine ya kimkakati imeleta ajira na kuchangia kasi na chachu ya ukuaji wa uchumi hususani katika Jiji la Dodoma.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Mhe.Jenista Mhagama akipokea taarifa ya ujenzi wa jengo la Kiwanda cha Mpiga Chapa wa Serikali katika ziara yake ya kikazi ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa miundombinu katika idara zilizo chini ya ofisi yake.

Ameyasema hayo Agosti 3, 2023 alipokuwa katika ziara ya kikazi ya kukagua ujenzi wa Jengo la Mpigachapa Mkuu wa Serikali.

Jengo la Kituo cha Taifa cha Usimamizi na Uratibu wa Maafa, Jengo la Wizara ya Mipango na Uwekezaji, na jengo la Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu).

Waziri Mhagama alisema kuwa, ujenzi wa miradi hiyo mikubwa ya kimkakati inayoendelea imewezesha vijana wengi kupata ajira katika maeneo hayo, na kujiongezea pato binafsi sambamba na kuchangia ukuaji wa uchumi kutokana na manunuzi ya bidhaa zinazotumika katika mradi hiyo kufanyika katika viwanda vilivyopo nchini.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu),Mhe.Jenista Mhagama akipokea taarifa ya ujenzi wa Jengo la Wizara ya Mipango na Uwekezaji katika ziara yake ya kikazi ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa miundombinu katika Mji wa Serikali.

Alipokuwa katika jengo la Mpigachapa Mkuu wa Serikali, Waziri Mhagama alisema kuwa, mradi huo mkubwa umefikia asilimia 97 ambapo kiwanda hicho kitakapokamilika kitakuwa na hadhi na sifa ya kuwa ni kiwanda kikubwa kimojawapo cha Serikali,ambapo mashine mpya zimeagizwa na kiwanda hicho kitafanya kazi za ndani ya nje na nchi za Afrika Mashariki (EAC) pamoja na ukanda wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC).

"Sisi tumejipanga kwa matumizi ya ndani na nje pia, nimefarijika kuona ujenzi kwa awamu, hii ya kwanza umefikia hatua kubwa, na ujenzi wa ofisi umeanza na unaenda kwa kasi,"amesisitiza Waziri Mhagama.

Alipokuwa katika Kituo cha Taifa cha Uratibu na Usimamizi wa Maafa, Mhe.Mhagama alisema, ujenzi wa awamu ya kwanza ya kituo hicho pia umekamilika kwa asilimia 94 na kufafanua kuwa maghala mawili makubwa na ofisi za watumishi zimeshakamilika.

"Tunalo jukumu la kuhakikisha kwamba katika kituo hicho nchi inafikia malengo ya kitaifa na maono na maelekezo ya Mhe.Rais Dkt.Samia Suluhu Hassan na Serikali kwa ujumla,"alibainisha Waziri Mhagama.

Waziri Mhagama alisema kuwa, katika kituo hicho cha maafa kutakuwa na vitu vingine vingi ambavyo vinajenga dhana nzima ya uratibu na usimamizi wa maafa.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Mhe.Jenista Mhagama akipokea taarifa ya ujenzi wa Kituo cha Taifa cha Usimamizi na Uratibu wa Maafa katika ziara yake ya kikazi ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa miundombinu katika idara zilizo chini ya ofisi yake.

Pia kutakuwa na kiwanja ambacho kitakuwa kinasaidia utuaji na uondokaji wa helikopta ambazo zitaweza kwenda kwenye shughuli za maafa, kutakuwa na kituo cha tiba kitakachosaidia dharura za maafa hasa katika magonjwa ya milipuko na kitatumika pia katika masuala ya utafiti na tiba na kituo cha mafunzo kwa wataalam ambao watashughulika na usimamizi na uratibu huo wa dharura.

Waziri Mhagama pia alitembelea na kukagua ujenzi wa jengo la Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) pamoja na Jengo la Wizara ya Mipango na Uwekezaji katika Mji wa Serikali Mtumba, na kuagiza kuongezeka kwa kazi ya ujenzi ili majengo hayo yaweze kukabidhiwa kwa wakati.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge na Uratibu), Mhe.Jenista Mhagama akipokea taarifa ya ujenzi wa Jengo la Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera Bunge na Uratibu) katika ziara yake ya kikazi ya kukagua maendeleo ya ujenzi wa miundombinu katika Mji wa Serikali.(Picha na OWM).

Kwa upande wake Naibu Katibu Mkuu wa ofisi hiyo, Bw. Anderson Mutatembwa alisema, ofisi hiyo itasimamia kikamilifu maelekezo yote yaliyotolewa na Waziri Mhagama ikiwa ni pamoja na kuzifanyia kazi chagamoto zilizojitokeza na kuhakikisha zinatatuliwa kwa wakati.

Awali akizungumza katika ziara hiyo, Mwakilishi na Msimamizi Mkuu wa miradi ya Ujenzi kutoka Chuo Kikuu cha Ardhi Mhandisi Anania Saudeni alikiri kuyapokea maagizo ya Mhe.Waziri Mhagama na kuyatekeleza kwa wakati, kimkataba na kukamilika katika ubora kulingana na maelekezo na kuhakikisha kazi zinafanyika usiku na mchana na kuongeza nguvu kazi ya kutosha na usimamizi madhubuti.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news