Tanzania ina mengi ya kujifunza Afrika Kusini-Balozi Bwana

CAPE TOWN-Balozi wa Tanzania Jamhuri ya Afrika Kusini Mhe. James Bwana amesema Tanzania inayo mengi ya kujifunza kwenye Mkutano wa Uwekezaji wa Madini Barani Afrika wa Mining Indaba utakaofanyika kuanzia tarehe 5 hadi 8 Februari, 2024 nchini Afrika Kusini.
Mbali ya kuwa Balozi wa Afrika Kusini pia, Mhe. balozi Bwana anaiwakilisha Tanzania katika nchi za Jamhuri ya Botswana na Ufalme wa Lesotho.

Ameyabainisha hayo leo Februari 4, 2024 wakati akizungumza katika mahojiano maalum baada ya kuzungumza na Ujumbe wa Tanzania unaotarajia kushiriki katika Mkutano huo utakaofanyika katika Hotel ya Westin ambapo mwaka huu unatimiza miaka 30 tangu kuanza kwake.
Amesema,Tanzania ikiwa miongoni mwa nchi zenye utajiri mkubwa wa madini Afrika na duniani inatarajia kunufaika vilivyo kupitia mkutano huo na hususan kujifunza mengi kutoka katika nchi ya Afrika Kusini ambayo imepiga hatua kubwa katika masuala mbalimbali kwenye mnyororo wa shughuli za madini ikiwemo yanayohusu uwekezaji kwenye sekta ya madini, teknolojia shughuli za uongezaji thamani madini pamoja na namna nchi hiyo inavyosimamia sekta ya madini.

Aidha, ameongeza kwamba, mbali na kujifunza kutoka katika nchi ya Afrika Kusini na mataifa mengine, pia Tanzania inatarajia kuutumia mkutano huo kunadi fursa zake za uwekezaji zilizopo katika Sekta ya Madini.

''Wenzetu katika Jamhuri ya Afrika Kusini wamepiga hatua kubwa katika sekta ya madini kwa hiyo kama nchi tunayo mengi ya kujifunza kutoka kwao na kutoka kwa nchi nyingine zinazoshiriki mkutano huo.

Afrika Kusini ni miongoni mwa nchi duniani ambazo zinafanya vizuri katika Sekta ya Madini na Rasilimali Madini imechangia kuwafikisha hapa," amesema balozi Bwana.
Wakati mkutano huo unatarajia kufunguliwa rasmi kesho Februari 5, 2024, leo Mawaziri kutoka nchi mbalimbali za Afrika wanaosimamia masuala yanayohusu madini wanakutana katika Kongamano kujadili mambo mbalimbali yanayohusu Sekta ya Madini Barani Afrika.

Kwa upande wa Tanzania, Naibu Waziri wa Madini Dkt. Steven Kiruswa anaongoza ujumbe wa Tanzania katika kongamano hilo, akiambatana na Katibu Mkuu Wizara ya Madini Kheri Mahimbali, Balozi wa Tanzania nchini humo Mhe. Bwana, Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Msafiri Mbibo, Kamishna wa Madini Dkt. AbdulRahman Mwanga na Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Jiolojia na Utafiti wa Madini Tanzania (GST). Dkt. Mussa Budeba.
Tanzania inashiriki kwa mara ya kwanza katika mkutano wa Uwekezaji wa Mining Indaba kwa kushirikiana na Sekta binafsi inayowakilishwa na Chemba ya Migodi Tanzania ambapo kampuni mbalimbali zilizo chini ya mwanvuli huo zinashiriki.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news