Makamu wa Rais aongoza maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani na kampeni ya upandaji miti Kitaifa

LINDI-Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.Balozi Dkt. Emmanuel Nchimbi ameelekeza uongozi wa Mikoa yote nchini kuhakikisha jitihada za upandaji miti zinaendelezwa kwa kuwekewa mkakati mahsusi unaojumuisha makundi yote katika jamii na kuzingatia ikolojia ya maeneo husika, ikiwa ni pamoja na kuzuia uvamizi na uharibifu wa maeneo yote ya hifadhi ya misitu.
Makamu wa Rais, ametoa maelekezo hayo, wakati akifungua Maadhimisho ya Siku ya Misitu Duniani na Siku ya Upandaji Miti Kitaifa, iliyofanyika katika Uwanja wa Ilulu mkoani Lindi leo Machi 19,2026.

Amesema ni muhimu kuhakikisha wananchi wanaoishi jirani na misitu ya asili na mashamba ya miti wanapatiwa elimu endelevu kuhusu matumizi bora ya ardhi, udhibiti wa uchomaji moto holela, na usimamizi shirikishi wa misitu ya vijiji.
Aidha, Makamu wa Rais amehimiza umuhimu wa Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Taasisi ya Utafiti wa Misitu Tanzania (TAFORI) kufanya tafiti zitakazojibu changamoto mbalimbali ambazo wakulima wa miti wanakabiliana nazo, hususan zile zinazojitokeza kwenye misitu ya asili.

Amesema, tafiti hizo zijumuishe zile zinazohusu miti inayofaa kwa maeneo ya Mkoa wa Lindi na mikoa mingine nchini, ikiwa ni pamoja na miti dawa.

Makamu wa Rais amesema zoezi la upandaji miti linapaswa kuwa endelevu ambapo ameiagiza Wizara ya Maliasili na Utalii kupitia Mfuko wa Misitu (TaFF) kuwezesha miradi ya upandaji miti kwa kuanzisha mashamba ya miti ya vijiji na watu binafsi.

Aidha, ameitaka Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kuanzisha vitalu vya miche ya miti vya kutosha katika maeneo mbalimbali ya nchi, ikiwemo miti ya asili itakayopandwa katika maeneo mbalimbali.
Sambamba na hilo, amesema ni vema elimu ya kutosha itolewe kwa wananchi ili kutunza na kukuza miti hiyo.

Halikdhalika, Makamu wa Rais amesema, pamoja na faida lukuki za rasilimali misitu, bado kuna changamoto nyingi zinazoikabili, zikiwemo, utegemezi mkubwa wa rasilimali za misitu kwa uchumi na kipato kwa jamii kwa njia ya kuni, mkaa na mbao, idadi kubwa ya mifugo inayoingizwa katika hifadhi za misitu kwa ajili ya kutafuta malisho, matukio ya uvamizi wa hifadhi za misitu kwa shughuli za kibinadamu hususan makazi, kilimo na uchimbaji wa madini, pamoja na uwepo wa matukio ya moto ndani ya hifadhi za misitu.

Amesema, changamoto hizo na nyinginezo zimesababisha kiwango cha upotevu wa misitu nchini kuongezeka hadi kufikia hekta 469,400 kwa mwaka ambacho ni kiwango kikubwa sana kisichoweza kuendelea kuvumilika, na hivyo inahitaji kushirikiana kuhakikisha misitu inalindwa na kuhifadhiwa.

Vilevile, Makamu wa Rais amesema Kampeni ya upandaji miti kitaifa iliyozinduliwa leo ni sehemu ya jitihada za makusudi zinazochukuliwa ili kulinda hifadhi za misitu na kuongeza uwajibikaji katika uhifadhi wa mazingira pamoja na kutambua na kuunga mkono jitihada za Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan za kutunza mazingira, ambapo amekuwa kinara wa uhifadhi, mathalan, aliposheherekea siku ya kumbukumbu ya kuzaliwa kwake mwaka huu alipanda miti na kuhimiza Watanzania kufanya hivyo.

Amesema, ajenda ya upandaji miti, uhifadhi wa misitu na utunzaji wa mazingira kwa ujumla ni kipaumbele katika Taifa letu na utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi (2025 – 2030) ambayo inalenga kulinda rasilimali za ardhi, misitu, maji na viumbe hai kwa lengo la kutetea ustawi wa wananchi na ukuaji wa uchumi endelevu.
Makamu wa Rais, ameutaka uongozi wa Mkoa wa Lindi kuhakikisha maeneo yote ya misitu yaliyohifadhiwa ndani ya Mkoa huo yanaendelea kulindwa na kutunzwa. Aidha, amewataka skusimamia ili kuhakikisha vijiji vinakuwa na mipango ya matumizi bora ya ardhi ambayo inasimamiwa vema.

Kaulimbiu ya maadhimisho hayo Kitaifa ambayo ni “Misitu ni Uchumi Endelevu, Tuihifadhi kwa Maendeleo ya Taifa.’’, na ile ya Kidunia “Misitu na Uchumi” (Forests and Economies) zote zinachagiza kutambua umuhimu wa misitu na mchango wake katika kukuza na kujenga uchumi wa nchi.

Kaulimbiu ya kitaifa inaendana na mipango yetu ya Taifa, ikiwemo Dira 2050 pamoja na mikakati mingine yenye nia ya kuifanya Tanzania inufaike kupitia rasilimali za misitu, kwani misitu ina mchango mkubwa katika uhifadhi wa wanyamapori, ufugaji nyuki, utalii, kilimo, upatikanaji wa maji kwa matumizi nyumbani, viwandani na mashambani.
Tanzania inakadiriwa kuwa na eneo la misitu lenye ukubwa wa takriban hekta milioni 48.1 sawa na 55% ya eneo lote la nchi kavu. Katika eneo hili, hekta milioni 44.7 (93%) ni misitu ya uoto wa miombo na hekta milioni 3.4 (7%) ni Misitu ya Uwanda wa Chini, Milimani, Mikoko na Mashamba ya Miti.

Sekta ya Misitu inayojumuisha ufugaji nyuki na wanyamapori, ilichangia takriban 3% katika Pato la Taifa mwaka 2024, hivyo kuifanya kuwa miongoni mwa vichocheo muhimu vya maendeleo ya Taifa.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Know matter how large or small your business is, advertising here