NA DIRAMAKINI
WIZARA ya Madini imewataka wachimbaji na wadau wa sekta ya madini kuchukua tahadhari kutokana na mvua zinazoendelea nchini. 

Kwa mujiibu wa taarifa iliyotolewa leo Machi 25,2026 na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini, Wizara ya Madini imeeleza kuwa, hatari zinazoweza kutokea ni pamoja na kuporomoka kwa kuta za migodi, kujaa kwa maji ghafla, na uharibifu wa miundombinu ya uchimbaji.
Wizara imesisitiza hatua muhimu ikiwemo kusimamisha shughuli katika maeneo hatarishi, kuweka alama za tahadhari, kuimarisha mifereji ya maji, na kuhakikisha upatikanaji wa vifaa vya kinga na huduma za afya.
Wachimbaji wanatakiwa pia kufuatilia taarifa za utabiri wa hali ya hewa kutoka Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) na kupata taarifa mapema kutoka Ofisi za Madini za Mikoa.