LATRA yatangaza viwango vipya vya nauli kwa huduma za usafiri nchini

Marekebisho yahusisha mabasi ya masafa marefu, daladala, teksi mtandao na pikipiki mtandao

NA DIRAMAKINI

MAMLAKA ya Udhibiti Usafiri Ardhini (LATRA) imetangaza rasmi viwango vipya vya nauli kwa huduma mbalimbali za usafiri nchini, ikiwa ni sehemu ya maboresho ya udhibiti wa sekta hiyo.
Marekebisho hayo yanahusisha mabasi ya masafa marefu, mabasi ya mijini (daladala), pamoja na huduma za teksi mtandao na pikipiki mtandao.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na mamlaka hiyo, uamuzi huo umefanyika kwa kuzingatia kifungu cha 19 cha Sheria ya Mamlaka ya Udhibiti Usafiri Ardhini, Sura ya 413, kinachoiruhusu LATRA kupanga na kurekebisha viwango vya nauli na tozo za huduma za usafiri ili kulinda maslahi ya wadau wote, wakiwemo watumiaji na watoa huduma.

Katika viwango vipya vilivyotolewa, nauli za mabasi ya masafa marefu zimeainishwa kulingana na daraja la basi pamoja na hali ya barabara.

Kwa mabasi ya kawaida (ordinary), abiria atalipa Sh57.93 kwa kila kilometa moja katika barabara za lami, huku kwa barabara za vumbi nauli ikiwa Sh66.62 kwa kilometa.

Kwa upande wa mabasi ya daraja la kati (semi-luxury), nauli imepangwa kuwa Sh74.18 kwa kila kilometa moja katika barabara za lami, hatua inayolenga kuendana na ubora wa huduma zinazotolewa katika daraja hilo.

Aidha, LATRA imefanya marekebisho ya nauli kwa mabasi ya mijini (daladala), ambapo safari ya umbali wa hadi kilometa 10 sasa itagharimu Sh700.

Nauli hiyo itaongezeka kulingana na umbali wa safari, na kufikia kiwango cha juu cha Sh1,500 kwa safari ya kati ya kilometa 36 hadi 40.

Tangazo hilo limetolewa kupitia Gazeti la Serikali, na viwango hivyo vipya vinatarajiwa kuanza kutumika rasmi siku 14 baada ya kutangazwa kwake, kwa mujibu wa taratibu za kisheria.

Marekebisho haya yanatarajiwa kuwa na athari kwa wadau mbalimbali wa sekta ya usafiri, hususan katika kuimarisha uwiano kati ya gharama za uendeshaji na uwezo wa wananchi kumudu huduma za usafiri.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Know matter how large or small your business is, advertising here