MOROGORO-Tume ya Madini kwa ushirikiano wa Shirika la Maendeleo ya Umoja wa Mataifa (UNDP) pamoja na Taasisi ya Kuendeleza Uchimbaji Mdogo (FADev) wameendelea kutoa mafunzo kwa wachimbaji wadogo katika Mkoa wa Morogoro ikiwa ni mkakati wa Serikali kuwasaidia wachimbaji wadogo mradi unaofadhiliwa na UNDP.
Akiongea na wachimbaji wa madini ujenzi katika Mkoa wa Morogoro Afisa Program kutoka FADev, Bi.Rehema Mkuli amesema kuwa mafunzo hayo yamelenga wachimbaji wadogo wanaojihusisha na madini ya ujenzi na viwanda, hususani madini ya kokoto kwa lengo la kuboresha uelewa wao wa kitaalamu na kuhamasisha mbinu salama na zenye tija katika shughuli za uchimbaji.
Pia, Bi.Rehema amesema,wachimbaji hao wanajifunza juu ya mbinu za Msingi za Uchoraji wa Ramani za Kijiolojia (Basic Geological Mapping), Usanifu salama na bora wa mashimo (Safe and Efficient Pit Design)
Aidha, kwa upande wa wakufunzi kutoka ofisi ya Afisa Madini Mkazi wa Mkoa wa Morogoro, Mjiolojia Asifiwe Waksoni Ngala amewalezea wachimbaji juu ya Uchoraji wa ramani za kijiolojia, na kuwataka wachimbaji kujifunza zaidi juu ya utambuzi wa aina mbalimbali za miamba na kuelewa madini yanayopatikana ndani yake.
Ujuzi huu unasaidia kuongeza ufanisi katika utambuzi wa rasilimali, kupunguza uchimbaji wa kubahatisha na kuongeza tija katika shughuli za uchimbaji.






