KATIKA Mwaka wa Fedha 2023/2024, Serikali ilianza rasmi utekelezaji wa mkondo wa amali mashuleni, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa Sera ya Elimu na Mafunzo ya Mwaka 2014, Toleo la 2023, pamoja na Mtaala Mpya wa Elimu wa Mwaka 2023.
Utekelezaji wa mkondo huo ulianza kwa majaribio katika shule 39, zikiwemo shule 25 za Serikali na 14 binafsi, kwa lengo la kupanua wigo na kufikia shule zote zenye vibali vya kufundisha mkondo wa amali nchini.
Hatua hiyo inalenga kuweka mazingira wezeshi kwa wanafunzi kujifunza kwa vitendo na kupata ujuzi unaokidhi mahitaji ya jamii na soko la ajira.
Kwa kutambua umuhimu wa elimu inayowawezesha wanafunzi kupata ujuzi wa vitendo, Mamlaka ya Elimu Tanzania (TEA), kupitia Mfuko wa Elimu wa Taifa, imeweka kipaumbele katika ufadhili wa miundombinu na vifaa vinavyohitajika katika utekelezaji wa mkondo wa amali.
Miongoni mwa shule zilizonufaika ni Shule ya Sekondari ya Wasichana Korogwe, ambayo imepatiwa vifaa vyenye thamani ya zaidi ya Shilingi milioni 400 kwa ajili ya kufundishia amali mbalimbali zinazotolewa shuleni hapo.
Tags
Elimu
Habari
Mafunzo ya Amali
Mfuko wa Elimu wa Taifa
TEA Tanzania
Wiki ya Elimu Ujuzi na Ubunifu
